Friday, February 15, 2013



AJIRA ZA WALIMU NA MJADALA UNAOENDELEA CHUONI: JE BEDCP NA BEDPSY HAZITAMBULIKI?

 Ni mjadala unaoshika kasi ghafla baada ya waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi Dk. Shukuru kwambwa kutangaza nafasi za ajira kwa walimu,suala hasa sio tu ajira kutangazwa bali ni mgawanyo wa fursa hiyo kwa kada mbalimbali za ualimu.Lengo la makala ya hii si kujadili kiwango cha asilimia za kupanda au kushuka kwa uajiri katika tasnia ninayoiheshimu ya ualimu bali kuthamini namna ambavyo walimu wanafunzi waliopo vyuoni walivyopokea fursa hizo za wenzao, lakini hasa nitalilenga kundi la wakufunzi la wanasihi na wanasaikolojia hususani katika chuo kikuuu Teofilo Kisanji.
Hofu imetanda kuwa wanafunzi wa ushauri na saikolojia hawawezi kuajiriwa chini ya wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi,hili limekuja baada ya wanafunzi toka TEKU kutopata nafasi ya kazi hata mmoja kwa wale waliosomea kozi hizo,hoja ni kwamba je serikali haitambui kozi hizi? Au upya wa kozi hapa TEKU ndio chanzo?. Pamoja na kwamba ni maswali magumu yasiyo na majibu ya moja kwa moja pia tunapaswa kufanya utafiti wa kina juu ya sababu zilizoleta hali hii.
Kwa upande wangu nitajenga hoja mbili tu kuhusiana na suala hili alafu nitakaribisha mjadala.Hoja ya kwanza ni kwamba suala la wahitimu wakufunzi kukosa fursa za ajira linaigusa TEKU tu,tujiulize vipi kuhusu vyuo kama UDSM,SEKUCO,TUMAINI,UDOM  n.k. hapa tujenge swali la mjadala kwamba wahitimu kutoka vyuo hivyo wamepata nafasi hizo zinazolalamikiwa? Kama jibu ni hapana basi kuna haja ya kumtafuta mchawi.Pia hapa kuna jambo ambalo limeibuka kuwa kozi hizi hazitambuliwi na serikali…mimi sio msemaji wa wizara lakini nachoweza sema ni kwamba huu ni aina ya upotoshaji wa kijinga kabisa na kwa utafiti wangu niliofanya kwa kuchunguza ‘post’ za ualimu za miaka miwili nyuma ni kwamba wahitimu wakufunzi walipata ‘post’ za serikali ila kwa kuwa TEKU ilikuwa bado haijatoa wahitimu wa kozi hizi ndio maana haikuwa ‘stori’.
Hoja yangu ya pili ni kwamba kukosa kwa ‘post’ kwa wahitimu wakufunzi wa ualimu kutoka vyuo mbalimbali nchini na TEKU ikwemo iwe changamoto kwa wanafunzi waliobaki vyuoni na waweze kusoma alama za nyakati kuwa kuajiriwa kunategemea pia na vipaumbele vya serikali kutokana na mahitaji, hivyo basi waondokane na fikra mgando za kukaa na kusubiri ‘post’ kipindi wanapokuwa wamemaliza vyuo badala ya kujihusisha na shughuli nyingine hata kutafuta kazi kwenye taasisi mbalimbali zinazoshughulika na masuala waliyosomea.
Kuhitimisha niseme kwamba natambua kuwa kwa mfumo wetu serikali ndio mwajiri nambari moja kuhusu suala la ajira lakini pia tutambue kuwa changamoto katika soko la ajira ni pana sana vilevile ongezeko la vyuo vikuu limeongeza idadi ya wataalam katika kada yetu ya ualimu basi sisi walimu wa kisasa tuwe na fikra pambanuzi na kujiandaa kuendana na kupambana na soko la ajira ndani hata la kimataifa.
Nakaribisha mjadala.
Imeandaliwa na; Melkiory John
                            TEKU/BEDCP/101562
                             0655141602/0767141603

No comments:

Post a Comment